Thursday 26 May 2016

USICHOKIJUA KUHUSIANA NA ALIYEKUWA WAZIRI WA NYUMBA MAREHEMU SOITA SHITANDA

Kifo cha aliyekuwa mbunge wa Malava Soita Shitanda kimewaacha wengi na huzuni, huku viongozi wengi wakijitokeza na kutuma risala zao za rambirambi kwa familia, wakazi wa eneo bunge la Malava na wakenya wote kwa jumla kwa kumpoteza kiongozi huyo.

Wengi wamemtaja kama kiongozi shupavu ambaye alifanya kazi yake bila ubaguzi, na kwa uhodari wa kutajika.

Ungependa kujua ni kwa nini kiongozi huyo amemiminiwa sifa riboribo? Safiri nami nikujulishe.

Aliyekuwa mbunge wa Malava, Marehemu  Peter Soita Shitanda
Marehemu Shitanda alizaliwa tarehe tisa mwezi Novemba mwaka wa elfu moja kenda mia hamsini na tisa katika kijiji cha Kabras, Malava na kupashwa tohara mwaka wa elfu moja kenda mia sabini na mbili.
Alijiunga na shule ya msingi ya Tande huko Malava mwaka wa elfu moja mia tisa sitini na saba kabla ya kujiunga na shule ya upili ya Malava kwa kiwango cha O-Level alikosomea hadi mwaka wa elfu moja mia kenda sabini na saba.
Mwaka mmoja baadaye, Shitanda alijiunga na chuo cha ufundi cha Kenya na baadaye kufanya kazi kama mwanafunzi wa uhasibu kwenye afisi za mwanasheria mkuu.

Mwaka wa elfu moja mia tisa themanini na tatu, akajiunga na chuo cha Strathmore alikokuwa kwa miaka miwili na punde baada ya kutoka chuo, akafanya kazi katika vitengo tofauti vya uhasibu katika wizara ya fedha nchini Kenya.

Mnamo mwaka wa tisini na saba, Shitanda aliiacha kazi ya uhasibu na kuingilia siasa. Aliwania kiti cha ubunge katika eneo bunge la Malava na kumshinda aliyekuwa kwa wakati huo waziri wa afya na mbunge wa eneo hilo Joshua Angatia katika tiketi ya chama cha Ford Kenya, chama kilichokuwa na umaarufu sana katika eneo la magharibi.

Mnamo mwaka wa elfu mbili na mbili Shitanda aliwania tena kiti hicho na kushinda na kufanywa naibu waziri katika afisi ya rais Mstaafu Mwai Kibaki. Miaka mitatu baadaye, Shitanda aliteuliwa kama waziri wa nyumba.

Kwenye uchaguzi wa mwaka wa elfu mbili na saba, Shitanda aliwania na kushinda tena kiti cha ubunge cha Malava na kumfanya kuwa mbunge ambaye amewahi kuongoza eneo hilo kwa muda mrefu Zaidi tangu taifa la Kenya kunyakua Uhuru. Aliteuliwa tena waziri katika wizara ya nyumba mwaka uo huo.

Aidha, Shitanda aliwania kiti cha ugavana katika Kaunti ya Kakamega mwaka wa elfu mbili na kumi na tatu na kushindwa na Gavana wa sasa wa Kaunti hiyo Wycliffe Oparanya.

Kulingana na ripoti, kiongozi huyo amekuwa akiugua ugonjwa wa kisukari kwa miaka miwili hadi alipokumbana na mauti Jumanne tarehe ishirini na nne mwezi Mei mwaka huu.

Shitanda alifariki siku tatu tu baada ya kakake mkubwa Walucho Shitanda kuzikwa siku ya Jumamosi, tarehe ishirini na moja Mwezi Mei mwaka huu.
Kando na Walucho, marehemu Shitanda ana kaka wawili; Ngaira na Mwombe na dada watatu, wote wako hai. Amewaacha watoto wanne.

Rais Uhuru Kenyatta amemtaja kiongozi huyo kama aliyeipenda nchi na aliyejitolea katika kufanya kazi yake.

Yote tisa, Kumi? Mungu ailaze roho yake mahali pema.


Na Caleb Kisabuli

No comments:

Post a Comment